Biashara ya muziki.
Mwaka 2004 niliandika kitabu kuhusu biashara ya muziki. Kwa
wakati huo kitabu hicho “Introduction To Music Business”
kilishabihiana na mazingira ya wakati huo.
Miaka michache iliyopita, dunia ilitegemea mabadiliko
makubwa kwenye biashara ya muziki kutokana na kuingia kwenye mfumo wa dijitali
(digital). Upatikanaji wa bidhaa za muziki kupitia mtandao wa intaneti, ilikuwa
furaha kwa mtumiaji. Na urahisi wa kupata wimbo mmoja badala ya kununua toleo
lote la albamu fulani, na kwa gharama nafuu.
Katika suala la uchumi kwenye biashara ya muziki ni kipigo
kwa msanii. Labda kwa wasanii wakubwa na wenye uwezo wa kulazimisha mkataba
wenye makato ya juu.
Kwa uhalisia, kampuni ya uaandaji wa muziki ‘lebo’ – ni
mwekezaji. Unapokuwapo mkataba; lebo inabeba gharama za kurekodi, kusambaza na
kuitambulisha pia. Lebo inafanya hivyo kwa makubaliano ya makato kutoka kwenye
mauzo. Na huo ndio mfumo ulivyo, hadi
tulipofikia mfumo wa kidijitali.
(Kutoka Linkedin)
Ni dhahiri kuwa mfumo huo hauhakikishi ujazo wa mfuko
(kipato cha fedha) kwa msanii. Na wengi kwenye biashara ya muziki wanatambua
ukweli huo. Na wengi hao watakuambia kuwa kipato cha msanii kinapatikana
kupitia maonyesho. Mzunguko wote kutoka ‘kugundulika’, kurekodi kwenye studio,
kuandikwa na kusikika kwenye vyombo vya habari n.k. Lengo kubwa ni kutumbuiza
mbele ya washabiki.
Kwenye ushiriki wa mzunguko huo, msanii na wadau wengine
wanakuwa na nia moja ya kufanikisha lengo hilo. Lakini siasa na uchumi wa
biashara ya muziki ni kikwazo cha kushindana na msanii muda wote.
Kama tukitoa upendeleo kwa msanii, teknolojia itakuwa
imemsaidia. Teknolojia ilivyobadilika, imemuwezesha kuwa na mawasiliano ya moja
kwa moja na wanaomfuatilia. Pia uwezo wa kufikisha kazi zake kwenye macho na
masikio ya wengi. Bado, huo sio ukombozi kwa msanii. Maana huduma zinazopatikana
kwenye mtandao zimekuwa sehemu ya mfumo wa uchumi kwenye biashara ya muziki.
Kihistoria, zao la sanaa linategemea ‘muonjaji’. Kama
vilivyo vinywaji, mtumiaji anaanzia hatua ya kuonja kabla ya kukubali au
kukataa matumizi ya kinywaji hicho. Hapo zipo njia mbili kwa hilo zao la sanaa.
(i) kupotea kwenye mtandao au (ii) kufanikiwa kwenye ushindani.
Kwa kuwa biashara ya muziki ni kama biashara nyingine
yeyote, mabadiliko yeyote yatawafanya wadau kubuni mbinu tofauti za kukabiliana
na mabadiliko hayo.
Zile lebo zilizokuwa zinategemea santuri kwenye mfumo
uliopita; ni hao waliojipenyeza kuunda huduma za usambazaji kidijitali.
(Kutoka SlideShare)


No comments:
Post a Comment